Wednesday, July 13, 2011

Mashujaa Musica yahangaikia mbili ili kukamilisha albamu ya pili.

Huku ikiendelea kukamilisha albamu ya pili, bendi ya Mashujaa Musica iko mbioni kumalizia nyimbo mbili za mwisho ili kukamilisha albamu ya pili ambayo inaandaliwa na bendi hiyo inayojiita 'Wana Posoposo'.
Rais wa bendi hiyo Jado Field Force alizitaja nyimbo hizo zinazofanyiwa na mazoezi na wanamuziki wa Mashujaa Musica kuwa ni 'Shukrani' na 'Mahakama ya Mapenzi'.
Wakati bendi hiyo ikiendelea na mazoezi ya kumalizia nyimbo hizo mbili, Jado alisema tayari wamesharekodi nyingine tatu ambazo amezitaja kwa majina ya 'Hukumu ya Mnafiki', 'Uchungu wa Moyo' na 'Lucia'.
"Kwa ujumla ni kwamba tuna nyimbo za kutosha albamu nzima lakini tunarekodi tatu na sasa tunaendelea kufanyia mazoezi nyingine mbili za mwisho huku zikiwepo zilizokamilika lakini hazijarekodiwa," alisema Jado.
Aliutaja wimbo wa 'Ulishawahi Kwenda kwa Mkweo' kwamba ni mojawapo ya zilie zilizokamilika lakini hazijarekodiwa ambapo utarekodiwa pamoja na hizo za  'Shukrani' na 'Mahakama ya Mapenzi' zinazoendelea kufanyiwa mazoezi.
Alisema ana uhakika kufikia mwishoni mwa mwezi huu Mashujaa Musica itakuwa imekamilisha nyimbo zote za albamu ya pili na kwamba itakuwa imebaki kazi ya kurekodi na kushuti video.
Rais huyo alisema kuwa kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa bendi hiyo imekuwa ikitamba na albamu ya kwanza ya 'Safari Yenye Vikwazo' na kufafanua kuwa ni wakati muafaka kuandaa albamu nyingine ili isaidie kuitambulisha zaidi bendi hiyo.
"Tunaendelea kujipanga vizuri zaidi kwa ajili ya kuteka soko la muziki wa dansi hapa nchini ndio tunaandaa nyimb kali zaidi ambazo tuna uhakika kwamba zitawavutia zaidi mashabiki wa muziki wa dansi," alisema.

No comments:

Post a Comment